Saturday, January 20, 2018

Kushamiri kwa Migogoro ya Ardhi Nchini



Makala:

Zikiwa zimepita siku chache tangu vikao vya Kamati za Bunge vianze mjini Dodoma hali ya mambo katika maeneo mbalimbali nchini si shwari kwani kumezuka mijadala mikubwa kutokana na madhira yaliyowapata wananchi kutokana na kupigwa,kuporwa mali ,kujeruhiwa kwa risasi za moto na Askari wakati wa utekelezaji wa operesheni za kuwaondoa wananchi wanaokaa katika maeneo yanayodaiwa kuwa ni Hifadhi pamoja na Ardhi inayodaiwa kutengwa kwa ajili ya Uwekezaji nk.

Vikao hivyo vilianza jumatatu ya tarehe 15 januari 2018,hii ikiwa ni kabla ya kuanza kwa Mkutano wa kumi wa Bunge,shughuli zilizopangwa kutekelezwa katika kipindi cha vikao hivi ni pamoja na ziara za ufuatiliaji ,uchambuzi wa miswada mbalimbali na kupokea maoni ya wadau pamoja na kupokea taarifa za utendaji za Wizara.

Kamati tatu za kisekta ambazo zitakuwa na jukumu la uchambuzi wa miswada mbalimbali ni pamoja na Kamati ya Sheria,Kamati ya Ardhi,Maliasili na Utalii pamoja na Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii.

Maoni yangu kwa wadau na wajumbe wa Kamati hizi watumie muda huu kuangalia namna ya kutatua tatizo lililomuelemea Mheshimiwa Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi  Wiliam Lukuvi ambaye kama angekuwa si Kiongozi Mahiri huenda Rais Magufuli angekuwa ameshamuweka pembeni kutokana na malalamiko likuki yanayoiandama Ofisi (Wizara)yake.

Kipekee niwapongeze Mawaziri hawa wawili Mheshimiwa Wiliam Lukuvi na Naibu wake Mheshimiwa Angelina Mabula kwa kazi kubwa wanayofanya ikiwemo kupokea na kufanyia kazi malalamiko takribani nchi nzima.

Ukweli Wizara hii ni ngumu,ina mianya mingi ya rushwa ambayo kama si umahiri wa Mawaziri hawa huenda Mahakama na Mabaraza ya ardhi kungefurika mafaili ya malalamiko zaidi ya haya,lakini kutokana na uchunguzi nilioufanya naona kabisa na ninaweka bayana kuwa Mawaziri hawa wamejitoa muhanga kwa ajili ya kupigania haki za wananchi wanyonge.


katika mkutano wa tisa wa bunge la kumi na moja November 16, 2017 akijibu maswali ya papo kwa papo Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhshimiwa Khasim Majaliwa aliulizwa maswali na wabunge Magdalena Sakaya (Kaliua) aliyetaka kujua Serikali imejipangaje kukabiliana na tatizo la mabadiliko ya tabia nchi suala ambalo ni la kidunia.

Katika majibu yake Waziri Mkuu alisema,
“Mheshimiwa Spika,mabadiliko ya tabia nchi yaliyokumba dunia na Tanzania ikiwemo,tunaendelea kukabili changamoto kwa  kuweka mipango mbalimbali kuhakikisha kuwa tunakabiliana na mabadiliko hayo,moja ya mikakati hiyo ni kusimamia Sheria ya uhifadhi wa Mazingira ili kuhakikisha Mazingira yanabaki yanasaidia kufanya mabadiliko ya hali ya hewa ya nchi yanabaki kuwa ya kawaida yanayowezesha binadamu au viumbe hai vyote ndani ya nchi kufanya kazi zake vizuri na kupata mahitaji yake vizuri”

Waziri Mkuu pia alisema kuwa Serikali imeendelea kusimamia Sheria za mazingira ambazo pia zinakinga maeneo mbalimbali hii ni pamoja na misitu,mito na maeneo mengine yote ili kukabiliana na hali hiyo.

Serikali pia imeendelea kutoa elimu kwa jamii kuwaelimisha Watanzania umuhimu wa Kutunza mazingira yetu kwa ujumla,zikiwemo taasisi za kimataifa zimeendelea pia kusaidia kupambana na tatizo hili.

Waziri Mkuu alitoa wito kwa watanzania nia wote kutunza mazingira na kwamba mabadiliko ya tabia nchi duniani hayatafanikiwa iwapo tutaendelea kuharibu misitu yetu,kuharibu vyanzo vyetu,tunaweza kukosa huduma za jamii zinazotokana na mabadiliko ya tabia nchi,hivyo ni muhimu sana kushirikiana na wataalamu kwa pamoja na wananchi wanaoishi na kila mmoja aliyepewa dhamana katika maeneo yao ili kuweza kushiriki kwa pamoja kuhifadhi Mazingira yetu.

Waziri Mkuu pia aliulizwa swali na Mheshimiwa Vedasto Edgar Ngombale (CUF) kuhusu shambulio lililofanywa julai 2017 na Askari Polisi ndani ya msikiti ambapo shambulio hilo lilipelekea kifo cha Shekh Ismail Weta na kuondolewa jicho kwa Shekh Abdalah Nakindabu ambapo Mbunge huyo alitaka kujua kama Serikali ina mpango wa kulipa fidia  kwa watu hao.

Akijibu swali hilo Mheshimiwa Waziri Mkuu alisema kuwa kwanza sina uhakika kama Askari walimshambulia mtajwa hapo na kumtoa jicho lakini jukumu la vyombo vya dola na Jeshi la Polisi likiwemo ni kulinda usalama wa raia na mali zao,si jukumu la polisi kwenda kumshambulia mtu na hatimaye Serikali ianze kufikiria kumlipa mtu fidia kutokana na shambulio lililofanywa na Askari Polisi na kama kuna Askari yeyote amefanya tendo hilo yeye mwenyewe nje ya majukumu yake ya kazi atachukuliwa hatua kama yeye aliyetenda kosa hilo.

“Serikali haiwajibiki kulipa fidia ikiwa si sehemu ya maagizo na wala si jukumu la majeshi ya vyombo vya dola bali ikithibitika mmoja kati ya watumishi wa vyombo vya dola ametenda kosa hilo na ikathibitika hivyo,yeye mwenyewe atawajibika kuchukuliwa hatua kali na ili kama kutakuwa na kulipa fidia itakuwa ni moja ya adhabu ambayo itatolewa na vyombo vinavyotoa hukumu”.alisisitiza Waziri Mkuu.

“Kwa hiyo Mheshimiwa Spika niseme tu kwamba,Serikali wala vyombo vyake vya dola havilengi kufanya kazi ya kuwatendea makosa wananchi bali ni kuwalinda wananchi pamoja na mali zao kama tulivyojipanga kufanya kazi”alisema Waziri Mkuu.

 Swali lingine ambalo nimelenga kulitumia kuthibitisha mambo yanayoashiria  kushamiri kwa migogoro ya Ardhi nchini liliulizwa mbele ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa Ulyankulu Mheshimiwa Kadutu kuhusu kuzuiwa kwa wananchi kufanya shughuli za kilimo na ufugaji huku maeneo hayo yakiwa yamepimwa na vijiji vyake vimeandikishwa na wananchi wakiwa na (GN) Tangazo la Serikali.

Akijibu swali hilo Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano Khasim Majaliwa alisema nchi yetu ina mapori yaliyohifadhiwa kisheria,yana mipaka yake rasmi kwa mujibu wa Sheria zinazoyalinda,mapori haya yapo katika kila eneo,na ni budi kila mtanzania kushiriki kuyahifadhi,kumetokea uvamizi unaofanywa na waliojirani na maeneo hayo,ni kweli maeneo hayo yamekuwa na migogoro mingi kati ya mapori yetu na vijiji,kati ya mapori na wananchi ambao wanaoenda kufanya shughuli za kijamii huko ndani ambapo pia Serikali hairuhusu kufanyika kwa shughuli za kijamii.

Kutokana na migogoro hii ya muda mrefu,Waziri Mkuu alitoa agizo kwa Wizara ya Maliasili na Utalii kufanya mapitio ya mipaka na kuweka alama kwenye mipaka ya mapori yote.

Kilichobainika,Serikali ilikuwa imeshasajili vijiji hivyo na kulianza migogoro hiyo baada ya wataalamu walioanza kwenda kufanya kazi ya kubaini mipaka katika mapori hayo tuliwasihi wananchi walio kwenye vijiji vilivyo ndani ya mapori hayo wawaache wataalamu wafanye mapitio na waweke alama hizo zinazobainisha mipaka ya ramani baada ya hapo Serikali itakuja kuona ni kijiji gani kilicho ndani na je pale palipo kijiji malengo yetu ya uhifadhi yamefikiwa na bado ni Mahitaji sahihi ili baadaye tuje kufanya maamuzi ya au kupunguza maeneo ambayo kwa sasa kwa uhifadhi huo hauna tija ili kuondoa migogoro.

Waziri Mkuu alisema kuwa kazi hiyo inaendelea na aliagiza kuwa ifikapo tarehe 30 mwezi wa kumi na mbili 2017 wataalam hao wawe wamekamilisha kupima mapori ambayo bado  baada ya hapo Serikali iangalie ni vijiji vingapi vilisajiliwa na Serikali na viko ndani ya hifadhi/mapori hayo na kama vijiji hivyo bado viko kwenye maeneo yaliyo na tija kwa malengo ya uhifadhi au la ili Serikali itoe maamuzi mengine.

Waziri Mkuu alitoa wito kwa wananchi ambao wako kwenye hifadhi ambazo zimetambuliwa baada ya uwekaji wa alama uliofanywa na wataalam waendelee na kazi hiyo baada ya kazi hiyo Serikali ifanye mapitio na kufanya maamuzi kwa maslahi ya nchiikiwemo kufuta kijiji au kubadilisha mipaka ambapo mpaka hapo Mahusiano kati ya Serikali na wananchi yatakuwa yameenda vizuri na wananchi watashiriki kulinda mapori na hifadhi hizo.  
Nakubaliana na majibu ya Mheshimiwa Waziri Mkuu Khasim Majaliwa,sasa kero zilizoko katika maeneo mbalimbali Nchini ni namna wahusika walioagizwa kufanya kazi hiyo walivyogeuza zoezi hilo kuwa uwanja wa vita!

Iwapo Serikali imeweza kubaini mapungufu yaliyosababishwa na watendaji mbalimbali wa Serikali katika Taasisi zake kikiwemo Chuo Kikuu cha Dar Es salaam kuingia mikataba vivyo hivyo wapo watendaji wa Serikali walioamua kufanya wanayotaka katika agizo hili la Mheshimiwa Waziri Mkuu hivyo ,kamati ya Maliasili ifuatilie maeneo mbalimbali na maeneo ya kuanza nayo iwe ni Mikoa ya Tabora na Katavi ambapo mpaka hivi sasa vikao vya Kamati za Bunge vinavyoendelea vinaweza kuona ni jinsi gani watendaji wakiwemo wateule wa Mheshimiwa Rais walivyofanya unyama kwa wananchi wa maeneo hayo bila huruma kwa kuchoma vyakula,nyumba,na mali mbalimbali za wananchi jambo linalofanya wananchi waingie mgogoro na Serikali bila sababu.

Kuna aibu kubwa juu ya mambo waliyofanyiwa wananchi kwani wananchi wamefikia hatua za kutozwa fedha kiasi cha shilingi laki moja kabla hata ya utaratibu ulioelezewa vizuri na Mheshimiwa Waziri Mkuu ambapo ingefanyika hivyo,wananchi wasingeweza kupata madhara kiasi cha kusababishwa kwa vifo ,majeruhi,upotevu wa mali na kukosa makazi na aibu ni kwa vijiji vilivyosajiliwa.

Kwa kauli nzuri iliyotolewa na Mheshimiwa Waziri Mkuu ni kwamba atambue kuwa viongozi wa Serikali ngazi za chini wamekuwa wakifanya vitu vya kushangaza mpaka wananchi wanajiuliza wana haki gani kwa Serikali yao waliyoiweka madarakani ambapo baada ya muda imekuwa ikiwageuka na kuwaona hawana thamani.

Itambulike kwa ujumla wake kwamba katika zoezi la kuweka mipaka maeneo ya mapori hakukuwa na ushirikishwaji kwa wananchi katika mambo haya ikiwemo matumizi bora ya ardhi haukufanyika hivyo yote yaliyofanyika kuhusu utesaji,uporaji na mengine ilikuwa ni hulka kwa wateule wa Rais ambao walilewa madaraka na kuamua kufanya watakavyo jambo lililosababisha familia za wananchi katika maeneo mbalimbali nchini kuishi maisha magumu ikiwamo kutokuwa na makazi,huduma za kijamii nk.

Nashauri viongozi wakuu wa Kitaifa waweke utaratibu mzuri wa kufuatilia maagizo waliyotoa ili kuona utekelezaji maana pindi wanapoondoka katika maeneo hayo viongozi wa chini yao hugeuka miungu watu na kusahau maelekezo waliyopewa.

MWISHO.




Serikali Yapiga Marufuku Kulima Pamba kwa Mkataba



Zao la Pamba likiwa Shambani picha na Maktaba.
WAZIRI MKUU wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa amesema Serikali imekataza kilimo cha pamba cha mkataba kwa sababu kinawanyonya wakulima.
Waziri Mkuu ameyasema hayo jana (Ijumaa, Januari 19, 2018) wakati akizungumza na wananchi baada ya kukagua zahanati ya Hunyari wilayani Bunda, akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Mara.
“Ni marufuku kwa wanunuzi wa pamba kulima pamoja na wakulima kwa sababu wakulima wanakosa uamuzi wa kupanga bei. Kuanzia sasa zao hilo litauzwa kwa njia ya mnada.”
Alisema Serikali imeweka mkakati wa kuimarisha mazao makuu ya biashara ambayo uzalishaji wake umeanza kupungua likiwemo na zao la pamba.
Waziri Mkuu alisema Serikali imeamua kushiriki kikamilifu katika usimamizi wa kilimo cha zao la pamba kuanzia hatua za maandalizi ya shamba, pembejeo hadi masoko.
Pia Waziri Mkuu amewaagiza Maofisa Kilimo katika wilaya hiyo wawafuate wakulima vijijini kwa ajili ya kutoa elimu itakayowawezesha wakulima kulima kwa kufuata njia bora za kisasa.Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka wafugaji kuhakikisha wanakuwa na idadi ya mifugo kulingana na uwezo wa eneo lao.“Marufuku kulisha mifugo katika mashamba ya watu.”
Amesema Serikali itachukua hatua kali za kisheria kwa mfugaji yeyote atakayelisha mifugo yake katika mashamba ya wakulima kwani tabia hiyo huchangia migogo baina yao.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU
Source: MCHAMBUZI BLOG / 16 minutes ago



Friday, January 19, 2018

HABARI ZA KISIASA ZILIZOTIKISA MWAKA 2017 MKOA WA SHINYANGA


Na Antony Sollo Shinyanga.
Mbwembwe pamoja na ushangiliaji wa aina yake zilivyotawala katika Uchaguzi  ndani ya Chama cha Mapinduzi Mkoani Shinyanga kwa mwaka 2017.

Wahenga walishasema,ukitaka uhondo wa Ngoma ingia ucheze!!!!!!

Hivi ndivyo ilivyokuwa katika uwanja wa siasa ndani ya CCM Mkoani  Shinyanga  ambapo wanachama wa chama hicho walibuni mbinu ya kuhamasisha namna ya kumpata Mwenyekiti wa Chama hicho Mkoani humo ambapo ilikuwa ni burudani tosha kwa watazamaji wa Uchaguzi wakiwemo waandishi wa Habari.

Kabla ya Uchaguzi na hatua ya kutangaza matokeo ya Uchaguzi ndani ya CCM Mkoani shinyanga kuliibuka mbwembwe na ushangiliaji wa aina yake ambao hautakaa usahaulike.
Mmoja wanachama wa Chama cha Mapinduzi waliotia fola kwa mwaka 2017 ni Mheshimiwa Diwani wa Kata ya Kiloleli Manyama.
iliyoko Wilaya ya Kishapu Mkoani Shinyanga 

Diwani huyo  alijizolea umaarufu baada ya kubuni mbinu ya kupiga kampeni akitumia chupa ya chai (Thermos) ambayo ilikuwa imetundikwa katikamoja ya nguzo na kila aliyekuwa akipita aliitikisa na hata kuibusu kama ishara fulani kuonyesha dira na mwelekeo wa mgombea waliyekuwa wameona ataweza kuivusha CCM katika Uchaguzi 2020.

Mwandishi wa Makala hii alifuatilia nini ilikuwa uhalisia juu ya chupa ya chai iliyokuwa imetundikwa kama mtindo mpya wa upigaji kampeni ambapo kupata ufafanuzi huo mwandishi alimtafuta Diwani wa Kata ya Kiloleli ambaye alikuwa na haya ya kuzungumza.
Mwandishi: Mheshimiwa Diwani naomba kufahamu ni kipi kilichopelekea mtundike chupa ya chai katika moja ya nguzo za hema iliyokuwa ndani ya ukumbi wa kupigia kura.

Diwani: ndugu mwandishi,hii ni mbinu mpya tuliyoibuni baada ya kukutana na kukubaliana namna gani tutaweka ishara kwa ajili ya kusaidia upigaji wa kampeni kwa mtu wetu ambaye tunaamini anazo sifa za kuivusha CCM katika chaguzi zijazo ukiwemo wa 2020.
Mwandishi:Mbinu hii imebuniwa na nani?
Diwani: “Mbinu hii nimeiasisi mimi,si unajua siasa ni ushindani na siasa kwa upande mwingine ni ubunifu? Sisi kama wapiga kura baada ya kukaa na kuwapima wagombea wetu walioomba kupigiwa kura tuliona nani atakisaidia chama kukifikisha pale tunapotaka na hasa kwa kuendana na kasi ya Mheshimiwa Rais yaani HAPA KAZI TU”

Mwandishi: kwa hiyo mlikuwa mnapiga kura mkijua ni wapi na ni nani anayeshinda?
Diwani: Hapana! Kutokana na mfumo wa Demokrasia,kila mtu anayo haki ya kuchagua mtu au kiongozi anayemtaka hivyo baada ya kupiga kampeni nikiwapa wazo langu wanachama kwa ujumla wao,tulikubaliana kuwa kwa wale watakaokuwa tayari kuniunga mkono juu ya maoni na mawazo yangu ishara kubwa ni kufika na kuibusu na kuitikisa chupa hiyo na ndiyo kilichotokea na baada ya kuona watu wengi wakipita na kuibusu na kuitikisa chupa niliona wazo langu limekubalika na jambo hili lilinifanya nielewe kuwa kazi ya hamasa niliyoifanya ilikuwa imezaa matunda!

Kutokana na uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa makala hii, Diwani wa Kata ya Kiloleli Manyama ameweza kuwa mwanasiasa wa mwaka 2017 aliyebuni mbinu ya kuweza kupata matokeo ya kile alichokibuni na kushinda kabla ya kutangazwa kwa matokeo jambo ambalo wengi hata wale ambao wanaweza kuhonga ili wapigiwe kura imekuwa vigumu kujua nai kampigia kura na nani hakumpigia kura mpaka baada ya matokeo ndipo wanapokuja kupata matokeo.

Katika Uchaguzi huo uliofanyika Desemba 5, 2017 katika uwanja wa CCM Kambarage Mjini Shinyanga,Mabala Mlolwa aliibuka kidedea baada ya kuwabwaga washindani wake ambapo Mlolwa alipata kura 702  John Festo Makune kura 35 na Cornel Ngudungi  akiambulia kura 02.

Msimamizi wa uchaguzi na mlezi wa Chama hicho Mkoani Shinyanga Abdallah Juma Magodi  ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar alimtangaza Mabala Mlolwa kuwa ndiye mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Shinyanga.

“Naomba kusoma matokeo ya kazi tuliyoifanya,Ndugu Mabala Mlolwa kura 702  Ndugu John Festo Makune kura 35 na Cornel Ngudungi kura 02.
“Hivyo kwa mamlaka niliyopewa ya kuwa msimamizi wa Uchaguzi huu namtangaza ndugu Mabala Mlolwa kuwa ndiye Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Shinyanga.”alisema Abdallah.

Kwa nafasi ya mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa ikichukuliwa na Gaspar Kileo  aliyepata kura 702 dhidi ya wapinzani wake Bernad Shigela aliyepata  kura 33 na
Joyce Masunga-02.







  
Wajumbe wakiwa wanaendelea na zoezi la upigaji kura katika ukumbi wa Uwanja wa Kambarage Mkoani Shinyanga.Picha na Antony Sollo

 Diwani wa Kata ya Kiloleli Mh Manyama akiwa na Diwani wa Viti Maalumu pamoja na Mbunge wa Jimbo la Kishapu Mh Suleiman Nchambi mwenye fimbo wakijadili jambo wakiwa na chupa ya chai iliyokuwa ndiyo kivutio cha wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga wakiwa kwenye Uchaguzi wa chama hicho Uwanja wa Kambarage Mkoani Shinyanga. Picha na Antony Sollo.








Mwenyekiti wa  CCM Mkoa wa Shinyanga  Mabala Mlolwa akiomba kura kwa wajumbe ili wampigie kura  kwa nafasi aliyoomba kuwa Mwenyekiti wa Chama Mkoa wa Shinyanga:  Picha na Antony Sollo



Mjumbe wa NEC Mkoa wa Shinyanga Mh Gasper Kileo akiwa na wajumbe wa Chama Mkoa waShinyanga kabla ya kujiuzuru kwa ajili ya kufanyika kwa uchaguzi -  Picha na Antony Sollo 



 Wajumbe wa Mkutano Mkuu wakiendelea na zoezi la kupiga kura katika ukumbi wa Mkutano uliofanyika ndani ya uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga Picha na Antony Sollo

 Mh Manyama Diwani wa Kata ya Kiloleli akionyesha ishara ya kunywa maziwa ikiwa ni ishara ya ushindi baada ya kuasisi mbinu mpya ya upigaji wa kampeni mbinu iliyovutia wengi.


 Maballa Mlolwa akiwa na wagombea  wa nafasi mbalimbali kabla ya Uchaguzi wa nafasi ya Mwenyekiti ambapo aliibuka kidedea na kufanikiwa kuishikilia nafasi ya Mwenyekiti wa Mkoa wa Shinyanga Picha na Antony Sollo

Mwenyekiti wa  CCM Mkoa wa Shinyanga  Mabala Mlolwa akitoa neno la shukrani kwa wajumbe walimpigia kura baada ya kuibuka mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti wa Chama hicho Mkoani Shinyanaga:  Picha na Antony Sollo

MWISHO.

Kwa Taarifa Matukio mbalimbali pamoja na matangazo wasiliana na Katibu wa TAMRA kwa namba 0762 116 116/ 0762 117 117/ 0785 118 118.
antonysollo5@gmail.com












Saturday, September 9, 2017

Wananchi Maganzo waiponda Kamati ya Ndugai.



·        Wasema iliacha kuangalia matatizo ya wananchi
·        Ilienda kwa ajili ya kuangalia madini pekee.
·        Wasema huo si uzalendo,Utaifa.
·        Kamati hiyo haikufanyi kazi Mgodi wa Elhilal ulioko hapo

Na Antony Sollo Shinyanga.
09.09.2017

WANANCHI wa Mji mdogo wa Maganzo Wilayani Kishapu Mkoa wa Shinyanga wametoa maoni yao kuhusu ripoti iliyowasilishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli huku wakiiponda Kamati iliyoundwa na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai wakisema Kamati hiyo ina mapungufu makubwa Tanzania Daima limeelezwa.

Akizungumza na gazeti hili mmoja wa wahanga wa mgodi huo George Joseph ambaye alipigwa risasi na walinzi wa mgodi huo ameilalamikia Kamati hiyo kwa kushindwa kuangalia maisha ya Raia na badala yake Kamati hiyo imedaiwa kujikita zaidi kuangalia wizi wa Madini ya Almasi katika Mgodi mmoja huku Mgodi unaomilikiwa na Phantom ambaye anamiliki Kampuni ijulikanayo kama Elhilal Mining ukiachwa bila kuchukuliwa taarifa zake yakiwemo mauaji ya wananchi wakazi wa Maganzo.

“ Ripoti ya Kamati hii ina mapungufu makubwa sana kwani ujio wake haukulenga kukutana na wahanga na pia ilipata makengeza kwa kushindwa kuuona mgodi wa Elhilal Mining unomilikiwa na Pantom ambapo Kamati hiyo imekutana na watu ambao taarifa zao zimejikita kwenye madini pekee lakini haikukumbuka kama kuna matukio makubwa ya Mauaji, unyanyasaji wa raia kama ilivyokuwa katika Kamati iliyoundwa kuchunguza zoezi la Operation Tokomeza ambapo Kamati hiyo ilizama zaidi katika masuala ya Haki za Binadamu kujua matatizo yiyowapata raia”alisema George.

George ameeleza kusikitishwa kwake na ubaguzi uliofanywa na Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Nyabaganga Talaba kwa kuwazuia waathirika waliopigwa risasi na walinzi wa Mgodi wa Mwadui kuingia katika kikao cha Kamati hiyo ili kueleza hali halisi na yanayojili kila siku katika Mgodi wa Mwadui na kwamba eneo la Mgodi wa Mwadui halimilikiwi na WDL pekee bali kuna mwekezaji mwingine ambaye amekuwa tishio kwa usalama wa raia kutokana na kuua vijana wengi na haku akilindwa na viongozi wa Serikali na hadi sasa hakuna hatua zilizochukuliwa dhidi yake.

“Mwekezaji huyu ameua watu wengi na viongozi wa Jeshi la Polisi na Madaktari waliokuwepo kipindi cha awamu ya Nne walikuwa na mnyororo mkubwa wa rushwa ambapo vijana wengi waliuawa na kupelekwa gerezani huku mmiliki wa Kampuni ya Elhilal akishinikiza vijana wanaokamatwa kupelekwa gerezani na kuwekwa mahabusu kwa lengo la kutukomoa,Phantom amediliki kunyang’anya maeneo ya watu lakini Serikali ilikuwa imewekwa mfukoni hebu tumuombe Mh Rais aje tumweleze mateso tuliyo nayo sisi wananchi wa Maganzo”alisema George.

Kwa mujibu wa George Joseph ambaye ni mmoja wa waathirika kutokana na kupigwa risasi na walinzi wa mgodi wa Mwadui  ni kwamba kuna makundi mbalimbali yaliyoachwa kusikilizwa na Kamati ya Ndugai na bila kuyataja makundi hayo ripoti hiyo inakuwa haijakamilika na inakuwa na doa lisilofutika.

Uchunguzi uliofanywa na Mwandishi wa gazeti hili umebaini kuwa Kamati hiyo ilipata kigugumizi cha kukutana na wahanga waliopata ulemavu kutokana na kushambuliwa kwa risasi za moto na walinzi wa Kampuni ya Zenity Security inayolinda rasrimali za mgodi wa Mwadui pamoja na walinzi wa Kampuni ya Elhilal Mining ambapo baada ya kulalamika sana wahanga hao waliahidiwa na Kamati hiyo kwamba wangekutana na Wajumbe wa Kamati hiyo Mjini Dodoma kabla ya kukabidhi Ripoti kwa Rais John Pombe Magufuli na sasa wanajiuliza! kwa kuwa Kamati hiyo imekabidhi ripoti hiyo bila kuwasikiliza watapata wapi tena nafasi ya kukutana ili waweze kueleza matatizo yao?


Katika hatua nyingine George na wenzake wamemuomba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufanya uchunguzi wa Viongozi wa Jeshi la Polisi waliokaa muda mrefu Mkoani Shinyanga maana kuna taarifa za kuwepo kwa namna Fulani ya ushirikiano kati ya taasisi za Serikali na Makampuni yanayofanya shughuli zake katika eneo la Mwadui.

“ kuna kesi nyingi za mauaji,kujeruhi kwa silaha za moto zimekuwa zikizimwa muda mrefu kwa ushirikiano wa madaktari wa Hospitali ya Serikali wakati wa uchunguzi wa majeruhi zikiwemo maiti baada ya mauaji yanayotokana na walinzi wa mgodi wa Mwadui na Elhilal inayomilikiwa na Phantom”.alisema George.

Ameyataja makundi hayo kama ifuatavyo.

Waliopigwa risasi na kupata ulemavu wa kudumu.

Katika kundi hili George anasema liko na watu wafuatao, yeye mwenyewe George Joseph Bwisige (alipigwa risasi na kupelekea kukatwa mguu wa kulia lakini hadi sasa hakuna hatua zozote zilizochukuliwa),Hamud Said , Marco Ngussa (ambaye alipigwa risasi na kupasuliwa bandama),Nyalulu Sitta (alipigwa risasi na kutobolewa jicho),

Kundi lingine ni la watu waliouawa kwa kupigwa risasi na Askari wa mgodi.

Hawa ni Benard Edward maarufu (Mayo), Shilagi Masali mkazi wa Masagala,Jishosha Daud, Hamad Shunda Mkazi wa Ikonongo ambaye hakuonekana isipokuwa nguo zake pekee tu ndiyo zilizoonekana

Hawa ni kundi dogo tu ambao taarifa zao zimeweza kupatikana na wengi wamepotelea katika mashimo yenye kina kirefu baad ya kukimbizwa wakielekezwa huko kwa lengo la kuwaua na wanamuomba Rais Magufuli aweze kuangalia utaratibu unaofaa ili kuwapatia kifut jasho waweze kukidhi mahitaji ya kibinadamu maana wamefanyiwa ukatili usiowezakusahaulika maishani mwao.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amekabidhiwa Ripoti Maalumu ya kuchunguza Biashara ya Madini ya Almasi na Tanzanite nchini 7 Agosti 2017 na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa tukio lililofanyika katika viwanja vya Ikulu jijini Dar es Salaam.

Kabla ya kukabidhiwa Ripoti hizo  kwa Rais Magufuli na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai alizipokea ripoti hizo kutoka kwa Wenyeviti wa Kamati Maalumu alizoziunda ambazo zilijumuisha Wabunge wa Bunge la Tanzania kutoka vyama mbalimbali vya Siasa.

Kamati hizo ziliongozwa na Dotto Biteko aliyeongoza Kamati ya kuchunguza biashara ya Madini ya Tanzanite na Mussa Azzan Zungu Kamati ya kuchunguza biashara za Madini ya Almas.

 Kamati hizo ziliundwa wakati wa Mkutano wa Saba wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ajili ya kuchunguza mfumo bora wa uchimbaji, usimamizi, umiliki na udhibiti wa biashara ya madini ya Almas na Tanzanite.

Akizungumza baada ya kukabidhiwa ripoti hizo, Rais Magufuli amemtaka Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwaita Wataalamu na Taasisi zote zinazohusika na masuala ya madini kufanya maandalizi ya kubadili Sheria zitakazosaidia Taifa kunufaika na rasilimali zake za madini.

 “ Huu ndiyo wakati wa kubadilisha sheria zetu. Mhe, Waziri Mkuu uwaite Wataalam wote wanaohusika na madini maandalizi haya yaanze haraka,” amesema Dkt. Magufuli.

Aidha, Rais Magufuli amesisitiza suala la uzalendo kwa Watanzania wote katika kusimamia rasilimali za nchi na kusema kuwa, ikiwa watanzania wataweka mbele uzalendo Taifa litasimama na kwamba hatutochezewa na wawekezaji tena na mikataba mibovu ambayo italiingizia Taif letu hasara.

Dkt. Magufuli amesema hivi sasa uchumi wa Tanzania unakua kwa asilimia 7 hadi 7.1 na nchi ya nne nyuma ya nchi ya Ethiopia ambayo uchumi wake unakua kwa asilimia 8.3 na kueleza kuwa, iwapo rasilimali hizo zingesimamiwa vizuri taifa lingenufaika zaidi na kuwa na uchumi zaidi ya nchi ya India ambayo haizalishi madini ya Tanzanite lakini imekuwa ni muuzaji mkubwa wa madini hayo.

 “ Tutangulize maslahi ya nchi yetu mbele,nataka tufike mahali tuanze upya,Mhe. Spika muendelee kutusaidia katika kusimamia rasilimali zetu, amesema Dkt. Magufuli.”

Katika hatua nyingine Rais Dkt. John Pombe Magufuli amewataka Wateule waliotajwa katika ripoti hiyo kukaa pembeni ili kupisha vyombo vya Ulinzi na Usalama kufanya kazi yake vizuri.

Rais Magufuli amesema hayo yote yanafanyika ili kuh akikisha kwamba watanzania wananufaika na rasilimali hizo na kueleza kuwa, bado watanzania hawajanuifa vya kutosha na rasilimali za nchi ikilinganishwa na rasilimali zilizopo.

Awali, akizungumza wakati wa kukabidhi Ripoti hizo, Waziri Mkuu Majaliwa alisema kuwa, Kamati mbili zilizoundwa na Spika wa Bunge zimefanya kazi kubwa na hali hiyo inatokana nia ya dhati aliyoionyesha Rais Magufuli kuhakikisha,rasilimali za madini zinakuwa na tija kwa Taifa.

 Kwa upande wake Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai alisema kuwa, Bunge liko tayari kuzipitia na kuzifanyia marekebisho Sheria zote ambazo hazilinufaishi Taifa na kueleza kuwa ipo haja ya kulifanyia kazi suala la mifumo ya udhibiti wa rasilimali hizo.

Ndugai amewataka viongozi wa Serikali waliopewa dhamana ya kusimamia shughuli za Umma kuguswa na umaskini wa Watanzania na hivyo kuzitaka Bodi mbalimbali nchini kubadilika na kuona haja ya kuangalia na kufuatilia kwa karibu maeneo wanayoyasimamia.

Akiwasilisha ripoti ya Madini ya Almasi Mwenyekiti wa Kamati hiyo  Mussa Azzan Zungu alisema soko la madini ya Almasi bado liko katika kiwango duni japokuwa Almas yenye thamani ya juu inapatikana Tanzania pekee.
a
 Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Tanzanite Dotto Biteko alieleza kuwa, asilimia 80 ya Tanzanite inatoroshwa nchini na asilimia 20 ya madini hayo ndiyo yanayoingia katika mfumo wa kodi nchini.


MWISHO.

Friday, September 8, 2017

Wachungaji wa Makanisa wadaiwa kuvamia Eneo la Shule


Na Antony Sollo Geita

Wachungaji wa Makanisa ya Grory of God, PVTC , CGT yaliyoko Mtaa wa Moringe Kata ya Buhalahala Mkoani Geita wameingia katika mvutano mkali na Uongozi wa Serikali ya Mtaa huo wakidaiwa kuvamia maeneo ya Shule ya awali ya Moringe Tanzania Daima linaweza kuripoti.

Licha ya Viongozi wa Makanisa hayo kuamuriwa kuondoka katika maeneo hayo na Mratibu wa baraza la Mazingira NEMC kutoka Halmashauri ya Mji wa Geita,Utekelezaji wa amri hiyo umekuwa ni mgumu kutokana na wachungaji hao kukaidi amri hiyo ambapo kanisa lililokuwa limeezekwa kwa maturubai sasa limeezekwa kwa kasi kwa kutumia bati.

Akizunguma na Tanzania Daima Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Moringe Adriano Rwechungura alisema kuwa,Viongozi hao wamekuwa wakiombwa mara kadhaa kuhama na kutafuta maeneo yanayofaa kwa kuendesha ibada zao lakini wameshindwa kuheshimu taratibu za Serikali na kuendeleza malumbano makubwa ambapo hadi sasa kuna mvutano mkubwa kati ya Serikali na taasisi hizo.

“Tumekuwa tukiwasihi viongozi hao wa Makanisa wafuate taratibu zilizowekwa na Serikali lakini hawataki na ni kwamba uwepo wa Makanisa katika eneo la Shule hiyo ni uvunjaji wa Sheria na ukwamishaji wa Maendeleo ya Sekta ya Elimu kwani kumekuwa na kelele nyingi zinazotokana na ibada zinazofanywa na waumini hao”alisema Rwechungura.

Kwa upande wake Msimamizi wa Shule ya awali ya Moringe Mwalimu Msafiri Masolwa alikiri kuwepo kwa kero katika eneo la Shule hiyo  na kusema kuwa Serikali itafakari juu ya mwingiliano wa taasisi hizo iwapo Shule au kanisa ibaki katika eneo hilo kufuatana na uhitaji wa wananchi wenyewe .

‘Taratibu ziangaliwe kwamba ni taasisi ipi ilikuwa ya kwanza kuanzisha shughuli zake katika eneo hilo na iwapo shule itaonekana ilikuwa ya kwanza ibaki na kama Kanisa lilikuwa la kwanza kuwepo katika eneo hilo basi hakuna budi kubakia katika eneo hilo alisema Masolwa”

Akizungumza na gazeti hili Katibu wa Tawi la Moringe kupitia Chama cha Mapiduzi Robert Maganga alisema kuwa katika  kulifuatilia suala wamekutana na mratibu wa baraza la Mazingira Mkoa wa Geita na kuambiwa kuwa,viongozi hao waliamuriwa kuondoka katika maeneo ya shule hiyo ndani ya siku saba lakini utekelezaji hujafanyika hadi sasa.

Kwa Mujibu wa  Rwechungura Wengine walioingia mgogoro na Serikali ya Mtaa wa Moringe ni pamoja na familia nne ambazo ziko katika eneo la Shule hiyo na kwamba zilishapewa notsi ya kupisha eneo la Shule na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Geita lakini wanafamilia hao walikataa kufanyiwa tathimini na kwamba Ofisi ya Mwenyekiti wa Mtaa inasubiri Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Geita atoe notsi kwa mara ya pili.

Kuhusu ujenzi wa barabara za Mtaa, Mwenyekiti wa Mtaa wa Moringe Adriano Rwechungura alimtuhumu Diwani wa Kata ya Buhalahala Elias Kabese kwa kuhujumu miradi mbalimbali ya maendeleo katika Mtaa wake.



“Diwani wetu hajatutendea haki kwani amehujumu miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa barabara kwamba March 2017 zilitolewa fedha za mfuko wa jimbo  na Mbunge wetu Mheshimiwa Costantine Kanyasu  kiasi cha shilingi mil 4 ambazo zilipangwa kwa ajili kuchongewa barabara kila Mtaa kwa masaa 8 lakini Diwani kwa sababu anazozijua yeye ameutenga Mtaa wetu na hadi sasa hakuna barabara hata moja iliyochongwa kupitia fedha za mfuko wa Jimbo zilizotolewa na Mbunge wetu na kwamba kufuatia hali hiyo ya kibaguzi iliyoonyeshwa na Diwani huyo wananchi wakazi wa Mtaa wa Moringe wameamua kuchangishana wenyewe na kwamba  Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Geita imekubali kutoa Greda  kwa ajili ya kuchonga barabara za Mtaa”.alisema Rwechungura.

Mbunge wa Jimbo la Geita Mjini Costantine Kanyasu alipotafutwa na Mwandishi wa gazeti hili ili kuzungumzia fedha za mfuko wa Jimbo alizotoa na tuhuma za ubaguzi unaofanywa na Diwani wa Kata ya Buhalahala Kanyasu likiri kutoa fedha hizo kwa ajili ya matengenezo ya barabara za Mtaa, lakini Mbunge huyo alionyesha wasiwasi wake kuhusu uadilifu wa Diwani huyo.

“ Usishangae ukisikia fedha hizo hazijafanya kazi iliyokusudiwa maana huyo bwana mdogo ni mjanjamjanja sana,sina uhakika kuhusu matumizi ya fedha hizo lakini kufuatia malalamiko hayo tutafanya utaratibu katika vikao vyetu vya halmashauri na ikibidi tutamtuma Mkaguzi wa ndani ili kwenda kujiridhisha juu ya matumizi ya fedha hizo na ikibainika kuwa kulikuwa na matumizi tofauti na malengo ya kutolewa kwa fedha hizo hatua stahiki zitachukuliwa”alisema Kanyasu.

Kanyasu ameliambia Tanzania Daima kuwa katika awamu ya pili atatoa kipaumbele kwa wakazi wa Mtaa wa Moringe kuwachongea barabara nzuri ili kuharakisha maendeleo yao.

MWISHO



Thursday, September 7, 2017

Mfanyabiashara Atuhumiwa kwa uchafuzi wa Mazingira




Na antony Sollo Geita
07.09.2017

MFANYABIASHARA Ernest Nyororo mkazi wa Geita analalamikiwa na wananchi kwa uchafuzi wa Mazingira ikiwemo kuathiri Afya za wananchi  kutokana na kusimika mashine za kusaga na kukoboa mpunga katika maeneo ya makazi  ya watu na kusababisha mvutano na viongozi wa Serikali ya Mtaa wa Moringe Tanzania Daima limeelezwa.


Akizungumza na Tanzania Daima Mwenyekiti wa Mtaa wa Moringe Adriano Rwechungura alisema kuwa Ofisi yake imejitahidi kusuluhisha jambo hili kwa kuiandikia barua Ofisi ya Mkurugenzi wa Mtendaji wa Mji wa Geita bila mafanikio ambapo hata hivyo walichukua hatua ya kumuandikia Mratbu wa NEMC Kanda ya Ziwa kwa hatua zaidi kwa madai kwamba Nyororo anatumia fedha zake kama fimbo ya kuwanyanyasa wananchi wanyonge.


“Sisi tumechukua hatua ya kumuandikia Mratibu wa NEMC Kanda ya Ziwa kutokana na jeuri ya mwekezaji huyu maana anatumia fedha zake vibaya kwamba tumeandika barua zaidi ya mara tano lakini hatuoni mabadiliko yoyote ambapo tumeona kila maafisa wanapoenda pale wananyamazishwa kwa fedha hatimaye tukachukua hatua hii”alisema Rwechungura

Tanzania Daima limepata nakala ya barua ya malalamiko yenye kumb Na NEMC/MZA/CMP/VOL1/49 iliyoandikwa na Mratibu wa baraza la Mazingira Kanda ya Ziwa kwenda kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji wa Geita ya tarehe 13/12/2016 ikikiri kupokea barua ya malalamiko kuhusu kero ya vumbi inayotokana na Mashine za kusaga na kukoboa mali ya Ernest Nyororo makazi wa Geita.

Katika barua hiyo,Mratibu wa NEMC Kanda ya Ziwa Jamal Baruti anamuagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji wa Geita kushughulikia kisheria suala hilo kwa kutumia kanuni na taratibu za Mazingira Mipango miji na Afya.

“Tunaomba suala hili lishughulikiwe kulingana na Sheria kanuni na taratibu za Mazingira Mipango miji na Afya kwani tunaamini kwamba utatuzi wa jambo hili ko ndani ya mamlaka ya Halmashauri”ilisema sehemu ya barua hiyo.

Kwa mujibu wa Kanuni na taratibu za Mazingira Maafisa wa Mazingira wa Wilaya na Miji wanayo mamlaka kamili ya kuhakikisha Sheria ya Mazingira ya 2004 inasimamiwa na kutekelezwa ipasavyo,aidha Maafisa wanaosimamia mipango miji na masuala ya Afya wanayo pia mamlaka ya kuhakikisha Sheria husika zinasimamiwa na kutekelezwa.

Hata hivyo Gazeti hili lilimtafuta Ernest Nyororo kuzungumzia mgogoro huo ambapo alikana na kusema kuna msuguano mkali dhidi yake na mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Moringe  Adriano Rwechungura ambaye Nyororo alidai kuwa Mwenyekiti huyo anatumia njia za kifisadi kutaka kumchafua.
“mimi sijakaidi maelekezo ya baraza la Mazingira isipokuwa kuna tatizo kubwa la kutokuwepo kwa maelewano na Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa Adriano Rwechungura amejificha nyuma ya jirani yangu ambaye hata hivyo nilipopewa maelekezo na watu wa NEMC kuziba mabati hapo kwenye eneo langu ndivyo nilivyofanya je walitaka nifanye nini zaidi?alihoji Nyororo.

Kwa upande wake Afisa wa Mazingira wa Halmashauri ya Mji wa Geita aliyefamika kwa jina moja la Shwekelela alipotafutwa kuzungumzia sakata hilo alisema yuko nje na Ofisi hivyo kuahidi atafutwe siku nyingine ambapo Tanzania Daima lilimtafuta tena kupitia namba ya mkononi 0785 909 308 ambapo simu hiyo iliita bila majibu na juhudi za kumtafuta zinaendelea.

MWISHO