Thursday, September 7, 2017

Mfanyabiashara Atuhumiwa kwa uchafuzi wa Mazingira




Na antony Sollo Geita
07.09.2017

MFANYABIASHARA Ernest Nyororo mkazi wa Geita analalamikiwa na wananchi kwa uchafuzi wa Mazingira ikiwemo kuathiri Afya za wananchi  kutokana na kusimika mashine za kusaga na kukoboa mpunga katika maeneo ya makazi  ya watu na kusababisha mvutano na viongozi wa Serikali ya Mtaa wa Moringe Tanzania Daima limeelezwa.


Akizungumza na Tanzania Daima Mwenyekiti wa Mtaa wa Moringe Adriano Rwechungura alisema kuwa Ofisi yake imejitahidi kusuluhisha jambo hili kwa kuiandikia barua Ofisi ya Mkurugenzi wa Mtendaji wa Mji wa Geita bila mafanikio ambapo hata hivyo walichukua hatua ya kumuandikia Mratbu wa NEMC Kanda ya Ziwa kwa hatua zaidi kwa madai kwamba Nyororo anatumia fedha zake kama fimbo ya kuwanyanyasa wananchi wanyonge.


“Sisi tumechukua hatua ya kumuandikia Mratibu wa NEMC Kanda ya Ziwa kutokana na jeuri ya mwekezaji huyu maana anatumia fedha zake vibaya kwamba tumeandika barua zaidi ya mara tano lakini hatuoni mabadiliko yoyote ambapo tumeona kila maafisa wanapoenda pale wananyamazishwa kwa fedha hatimaye tukachukua hatua hii”alisema Rwechungura

Tanzania Daima limepata nakala ya barua ya malalamiko yenye kumb Na NEMC/MZA/CMP/VOL1/49 iliyoandikwa na Mratibu wa baraza la Mazingira Kanda ya Ziwa kwenda kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji wa Geita ya tarehe 13/12/2016 ikikiri kupokea barua ya malalamiko kuhusu kero ya vumbi inayotokana na Mashine za kusaga na kukoboa mali ya Ernest Nyororo makazi wa Geita.

Katika barua hiyo,Mratibu wa NEMC Kanda ya Ziwa Jamal Baruti anamuagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji wa Geita kushughulikia kisheria suala hilo kwa kutumia kanuni na taratibu za Mazingira Mipango miji na Afya.

“Tunaomba suala hili lishughulikiwe kulingana na Sheria kanuni na taratibu za Mazingira Mipango miji na Afya kwani tunaamini kwamba utatuzi wa jambo hili ko ndani ya mamlaka ya Halmashauri”ilisema sehemu ya barua hiyo.

Kwa mujibu wa Kanuni na taratibu za Mazingira Maafisa wa Mazingira wa Wilaya na Miji wanayo mamlaka kamili ya kuhakikisha Sheria ya Mazingira ya 2004 inasimamiwa na kutekelezwa ipasavyo,aidha Maafisa wanaosimamia mipango miji na masuala ya Afya wanayo pia mamlaka ya kuhakikisha Sheria husika zinasimamiwa na kutekelezwa.

Hata hivyo Gazeti hili lilimtafuta Ernest Nyororo kuzungumzia mgogoro huo ambapo alikana na kusema kuna msuguano mkali dhidi yake na mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Moringe  Adriano Rwechungura ambaye Nyororo alidai kuwa Mwenyekiti huyo anatumia njia za kifisadi kutaka kumchafua.
“mimi sijakaidi maelekezo ya baraza la Mazingira isipokuwa kuna tatizo kubwa la kutokuwepo kwa maelewano na Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa Adriano Rwechungura amejificha nyuma ya jirani yangu ambaye hata hivyo nilipopewa maelekezo na watu wa NEMC kuziba mabati hapo kwenye eneo langu ndivyo nilivyofanya je walitaka nifanye nini zaidi?alihoji Nyororo.

Kwa upande wake Afisa wa Mazingira wa Halmashauri ya Mji wa Geita aliyefamika kwa jina moja la Shwekelela alipotafutwa kuzungumzia sakata hilo alisema yuko nje na Ofisi hivyo kuahidi atafutwe siku nyingine ambapo Tanzania Daima lilimtafuta tena kupitia namba ya mkononi 0785 909 308 ambapo simu hiyo iliita bila majibu na juhudi za kumtafuta zinaendelea.

MWISHO