Wednesday, February 14, 2018

Bundi atua Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu.

Na Antony Sollo Ushetu.
14.feb 2018

MGOGORO mkubwa umeibuka baina ya Emmanuel Makashi ambaye ni Diwani wa Kata na Christopher Rwagasanga Lyogelo ambaye ni Afisa Mtendaji wa Kata ya Sabasabini iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu Mkoni Shinyanga,hali iliyopelekea diwani huyo kuangua kilio katika kikao cha baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo akimtuhumu Afisa mtendaji huyokuhujumu shughuli za maendeleo ya Kata hiyo.

Akiwasilisha malalamiko yake mbele ya Madiwani hao kilichofanyika Februali 14 mwaka huu huko Ushetu Makashi lisema kuwa Afisa Mtendaji huyo amekuwa akibeza kila kitu kinachofanywa na Diwani huyo.

“Mheshimiwa mwenyekiti Afisa Mtendaji huyo amekuwa akichonganisha na wananchi huku akisema kwamba mimi sijasoma,na kuwaambia kuwa yeyendiye anafaa kuwa kiongozi wao akidai kuwa anashahada ya elimu ya juu na kuwaambia kwamba mimi sina uwezo wa kuwaletea maendeleo amekuwa akiwashawishi watendaji wa vijiji kutojishughulisha katika masuala mbalimbali ikiwemo uchangiaji wa shughuli za maendeleo”alisema Makashi.

Kutokana na uchungu aliokuwa nao Makashi aliangua kilio mbele ya viongozi mbalimbali waliohudhuria kikao cha baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo kilichoketi kwa lengo la kujadili mambo mbalimbali ya maendeleo ikiwamo miradi ya maendeleo kwa wananchi wa Ushetu.

Baraza hilo lilihudhuriwa na viongozi mbambli mbali wa Chama na serikali akiwemo mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga Mabala Mlolwa pamoja na katibu Tawala wa Wilaya ya Kahama, Timoth Ndanya ambapo Diwani huyo aliamua Mtendaji huyo kwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga huku akisema.

“Ndugu mwenyekiti kuna tatizo la kiutendaji katika Kata yangu ya Sabasabini kwamba, Afisa Mtendaji wa Kata amekuwa kikwazo kikubwa cha maendeleo kwa wananchi wangu, tangu aanze kazi kwenye Kata yangu mwaka 2016 hakuna maendeleo yoyote kwani amekuwa akiwagomesha wananchi kuchangia shughuli za maendeleo,” alilalamika Makashi.

Katika jitihada za kutatua mgogoro huo Makashi alimuomba Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo Matomola Michael kufika katika Kata hiyo ili kuwapatanisha waendelee kuwatumikia wananchi huku akisema tangu kuanza kwa figisu figisu za Afisa Mtendaji huyo hadi sasa hakuna kitu kinachofanyika kutokana na mgogoro huo.

“Mheshimiwa mwenyekiti kibaya zaidi Afisa Mtendaji huyo amekuwa akiwashawishi na watendaji wengine wa vijiji wasinipe ushirikiano katika kutekeleza shughuli za maendeleo kwa wananchi kwa madai kwamba yeye ndiye kiongozi sahihi kutokana na kwamba ana nashahada ya elimu ya juu,kwa kweli nakuomba Mkurugenzi aunde tume ya uchunguzi dhidi yake,kama hutafanya hivyo tubadilishane ofisi wewe uwe diwani na mimi nikae kwenye kiti chako cha ukurugenzi ili na wewe uone vitendo ninavyofanyiwa na Mtendaji huyo,” alisema Makashi kwa uchungu.

Makashi alisema kuwa,kabla ya ujio wa Afisa Mtendaji huyo katika Kata ya sabasabini, kulikuwa na mahusiano mazuri na  wananchi kutokana na ushirikiano mzuri kati yake na kaimu afisa mtendaji aliyekuwapo kipindi cha 2013 /2015 kwa kufanikisha kutimiza agizo la Rais Magufuli juu ya kutengeneza Madawati mashuleni ambapo walifanikisha kuchonga madawati 74 yaliyogharimu kiasi cha shilingi milioni 8.8

Makashi alisema kuwa katika kipindi hicho alijitolea katika ujenzi wa matundu ya choo cha shule kwa kuchangia kiasi cha shilingi 150,000 na kuongeza kuwa kiasi cha shilingi milioni 5.3 kilitumika kujenga nyumba ya mganga  katika Zahanati ya Kata huku nguvu ya wananchi ni shilingi milioni 1.2.

Makashi alibainisha kuwa katika kipindi cha mwaka 2017 alifanikisha kujenga barabara ya Sabasabini kwenda Iponyang’holo kiwango cha changarawe yenye urefu wa kilometa 9 kwa gharama ya shilingi milioni 2.5 kwa ushirikiano na diwani wake wa viti maalum Felista Nyerere ambaye alichanga shilingi 300,000 kati ya fedha hizo,ambapo alidai kuwa tangu mtendaji huyo aanze kazi shughuli za maendeleo zimesimama kutokana na mgogoro wao.

“Mtendaji huyo alianza kazi katika kata hii tangu mwaka 2016, na alinikuta nikiwa vizuri na wananchi wangu  lakini tangu aanze kazi nimeshindwa kumuelewa labda anaitaka hii Kata!, maana kinachofanywa na Mtendaji huyu ni uvunjaji wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano na ninaona Mtendaji huyu anapingana na kasi ya Mheshimiwa Rais kwa kuamua kukwamisha shughuli za maendeleo kwa makusudi,mimi naomba Mkurugenzi aunde hiyo Tume ili kuweza kutatua mgogoro huu vinginevyo Kata hii haitaweza kupata maendeleo”alisema Makashi.

Akichangia hoja hiyo Diwani wa Kata ya Bulungwa Joseph Masaluta alilieleza baraza hilo kuwa wote wawili kwa maana ya Diwani pamoja na afisa mtendaji huyo wa Kata wapelekwe kwenye kamati ya maadili kwa lengo la kuhojiwa kwa kina ili kubaini chanzo cha mgogoro wao na kuongeza kuwa wawili hao wamekutana wote ni jeuri.
Katika majibu yake kwa diwani huyo Makamu mwenyekiti wa baraza hilo Gagi Lala ambaye ndiye alikuwa akiongoza baraza hilo alisema,

“Mkurugenzi haiwezekani mtu alalamike kiasi hiki tena hadharani inaonekana kuna tatizo linalopaswa kushughulikiwa, pamoja na kwamba kanuni za baraza haziruhusu kuingiza taarifa zilizo nje ya shughuli za baraza , mheshimiwa diwani ujumbe umefika kuwa mtulivu tutalishughulikia suala hili,” alisema Lala.

Kwa upande wake kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu Benjamin Onesmo ambaye pia ni afisa maendeleo ya jamii katika Halmashauri hiyo alisema kuwa kutokana na hali hiyo ofisi yake imelichukua suala hilo na italitafutia ufumbuzi wa haraka.
“Mheshimiwa Mwenyekiti ofisi yangu inalibeba suala hilo na litashughulikiwa na kupatiwa ufumbuzi wa Haraka,” alisema Onesmo”.

MWISHO.